Saturday, September 1, 2012



                  MSUKUMA AOMBA KUNUSURU JAHAZI LA CCM GEITA.
                                Katibu wa itkadi na uenezi wa CCM Nape Mnauye.

Na Daniel Limbe,geita
ALIYEKUWA mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita,Joseph Musukuma amesema Chama cha mapinduzi mkoani humo kitafanikiwa kuzirejesha nafasi mbalimbali zilizotwaliwa na vyama vya upinzani iwapo atachaguliwa kushika nafasi ya uenyekiti wa chama hicho.
 
Msukuma aliyasema hayo jana muda mfupi baada ya kuchukua fomu ya kugombea nafasi ya uenyekiti wa CCM mkoa mpya wa geita ambapo alidai anakusudia kurejesha imani ya chama hicho kwa wananchi kutokana na baadhi yao kukisusia baada ya viongozi waliokuwepo awali kutokuwa na mvuto kwa wananchi.
 
Alisema CCM ni chama chenye maono mazuri kwa ajili ya kuwasaidia wananchi lakini baadhi ya viongozi wachache wamekuwa wakikivuruga chama hicho kutokana na kutaka kujipatia maslahi binafsi kinyume cha sheria huku wananchi waliowengi wakizidi kutaabika na ugumu wa maisha. 
 
Msukuma ambaye pia ni diwani wa Kata ya Nzera(CCM),alisema ameamua kuchukuwa fomu kuwania nafasi hiyo baada ya kuona wagombea wenzake wanaowania nafasi hiyo hawana sifa za kuongoza nafasi hiyo nyeti ndani ya chama cha mapinduzi.

Kufuatia hali hiyo alidai kushawishika kuomba nafasi hiyo mhimu ili kurejesha mshikamano na kukijenga chama hicho kwa kile alichodai kimepoteza sifa kutokana na baadhi ya viongozi kufanya kazi kwa mazoea na si kuwaletea maendeleo wananchi wa kipato cha chini hali ambayo imesababisha watu kukichukia na kukihama kila kukicha kwa kukimbilia kwenye vyama vingine vya upinzani.

“Nimelazimika kuchukua fomu ya uenyekiti Mkoa wa Geita baada ya kugundua wote walioomba nafasi hiyo wameshindwa kukiongoza maana wengi wao ni wale waliokuwa viongozi wa chama chetu ndani ya Wilaya na badala ya kukipeleka kwenye msitari kwa sasa kinaenda mlama hiyo ndiyo sababu kubwa ya mimi kuamua kuomba nafasi hiyo ili nikirudishe chama chetu kwenye msitari”
 
 
Kwa mjibu wa Katibu wa CCM mkoa wa geita Francis Elias tayari vigogo watatu ndani ya chama hicho akiwemo Musukuma wamechukuwa fomu za kuwania nafasi hiyo ambapo wengine  ni pamoja na Daud Ntinonu aliyewahi kuwa mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Geita,na nafasi yake kuchukuliwa na mwenyekiti wa sasa John Chenge Luhemeja ambaye naye anawania kiti hicho.
 
 
Musukuma aliondolewa kwenye nafasi ya uenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Geita na madiwani wenzake mapema mwaka jana baada ya kutuhumiwa kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutangaza hadharani majina ya mafisadi wa halmashauri ya geita na kuahidi kuwaburuza mahakamani pasipo kibari cha madiwani wenzake.

No comments:

Post a Comment