Wednesday, August 1, 2012

MADIWANI CHATO WAGEUKA MBOGO KUDAI GARI LA MKURUGENZI

Na Daniel Limbe,Chato
MADIWANI wa halmashauri ya Chato Mkoani Geita wamemtuhumu mwenyekiti na aliyekuwa mkurugenzi wa halmashauri hiyo Hamida Kwikwega kuficha gari la serikali kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa huku baadhi yao wakidai gari hilo limeuzwa kwa mtu binafsi kinyume cha sheria.
Wakizungumza kwenye kikao cha baraza jana madiwani hao waligeuka Mbogo,baada ya kumtaka Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo Charles Maisha kueleza mahali lilipouzwa gari jipya la halmashauri hiyo STK 5211 aina ya Toyota Land Cruser V8 lililonunuliwa na serikali kwa thamani ya zaidi ya Shilingi Milioni 200.
Hatua hiyo ilikuja muda mfupi baada ya Diwani wa kata ya Muganza Marco Maduka (CHADEMA)kuomba mwongozo wa Kanuni,na kisha kutaka baraza hilo kupewa taarifa juu ya mahali lilipo gari hilo ambalo ni mali ya halmashauri ya wilaya hiyo.
Awali gari hilo lilikuwa likitumiwa kwa ajili ya matumizi ya Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo,lilifanya kazi kwa muda wa miezi mitatu kisha ikadaiwa kwamba limeharibika Injini na kupelekwa katika moja ya gereji za kutengeneza magari jijini mwanza.
Hata hivyo baadhi ya madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo waligundua kupitia kwa raia wema kwamba gari hilo lilihujumiwa na baadhi ya watumishi wa serikali wakiongozwa na aliyekuwa Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kwa kunyofoa Injini yake na kuiuza kwa mtu binafsi kisha kuweka injini nyingine isiyofaa.
Kufuatia hali hiyo madiwani walikuja juu na kumtaka aliyekuwa mkurugenzi wa halmashauri hiyo (Hamida Kwikwega) kabla ya kuvuliwa madaraka na kuhamishiwa katika sehemu nyingine kikazi,kulirejesha gari hilo na hasa baada ya kubaini kuwa gari hilo lilikuwa limepelekwa kwenye Gereji ya Mumewe waliyoitaja kwa jina la M City.
Vile vile madiwani hao walilazimika kumweleza Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na serikali za mitaa (TAMISEMI)Agrey Mwanry wakati alipotembelea halmashauri hiyo mwishoni mwa mwaka jana katika ziara yake,na kudai kuwa gari hilo limefanyiwa njama za kuuzwa injini yake kwa lengo la kuwanufaisha watu wachache.
Katika sakata hilo Naibu Waziri alimsimamisha Mkurugenzi huyo na kumtaka kutoa maelezo juu ya tuhuma hizo ambapo alikiri kwamba gari hilo liliharibika Injini na hivyo kupelekwa Jijini mwanza kwa ajili ya matengenezo ingawa baadhi ya watendaji na hata madiwani hawakupatiwa taarifa.
Kufuatia hali hiyo Naibu Waziri alimuagiza mkurugenzi kuambatana naye hadi jijini mwanza lilipo gari hilo kwa ajili ya kulishuhudia na baada ya kuliona alimuagiza kulitoa kwenye gereji hiyo iliyokuwa ikidaiwa kuwa ni ya mumewe na kulipeleka TEMESA,hata hivyo lilipofikishwa huko ilibainika kuwa gari hilo halikua na injini yake halali.
Akizungumia sakata hilo katika baraza hilo Diwani wa kata ya Buseresere Chrispine Kagoma (Chadema) alisema taarifa za uhakika ambazo madiwani wamezipata ni kwamba TEMESA wamekataa kulitengeneza gari hilo kwa vile vifaa vingi vya gari hilo ikiwemo injini yake vimenyofolewa na kuuzwa.
“Taarifa sahihi tulizo nazo ni kwamba baada ya sisi kuibua ufisadi huo mbele ya Naibu Waziri,watendaji wanaodaiwa kuliuza gari hilo kwa harakaharaka waliamua kulirejesha gari hilo kwenye gereji ya mume wa aliyekuwa mkurugenzi ili lionekane linatengenezwa,lakini kumbe ilikuwa ni kiini macho,na kibaya zaidi pamoja na Waziri kuagiza lirejeshwe mpaka leo hii bado halijarejeshwa…’’ Alisema Diwani huyo kwa msisitizo.
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Ilemela Ismael Luge alisema hawako tayari kuona ufisadi mkubwa kama huo unaendelea kufanyika katika halmashauri hiyo huku wao kama wawakilishi wa wananchi wapo,ambapo alimtaka Mwenyekiti huyo kulirejesha gari hilo hata kama ni bovu ili liwekwe katika eneo la halmashauri hiyo.
“Mwenyekiti hatuko tayari kuendelea kuona vitendo vya kifisadi vikiendelea kufanyika kwenye halmashauri yetu,tunachotaka ni kuona hilo gari linarejeshwa hapa kwenye halmashauri yetu,ni bora lije hapa ili tuwe tunaliona tu inatosha vinginevyo kama haliji basi sisi tufanye maamuzi mazito,lakini kubwa tunahitaji kuliona gari hilo kwa sababu lina thamani kubwa na haliwezi kupotea kienyeji hivyo……’’ alisema Luge.
Akijibu hoja hizo za madiwani ambazo zilijadiliwa na zaidi ya madiwani zaidi ya watamo, Mwenyekiti wa halmashauri hiyo alionekana kutumia ubabe kuiondoa hoja hiyo ya madiwani kwa kueleza kuwa suala hilo linashughulikiwa na taarifa zake tayari zipo na kuamua kuufunga mjadala huo pamoja na kwamba baadhi ya madiwani waliendelea kunung’unika na kisha kuendelea na kikao kwa kujadili ajenda zingine.
Ni miezi minane sasa imepita tangu Naibu Waziri wa TAMISEMI Mwanry kuuagiza uongozi wa halmashauri ya wilaya hiyo kulirejesha gari hilo,ingawa hadi jana Jumatano lilikuwa halijarejeshwa na hakukuwa na majibu sahihi juu ya Gari hilo.
Halmashauri ya wilaya ya Chato ni miongoni mwa halmashauri zilizokumbwa na kashfa mbalimbali ikiwemo kuhujumu fedha za pembejeo za wakulima zaidi ya shilingi Bilioni 1.3,hali iliyopelekea serikali kuamua kuwawajibisha Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo kwa kumvua madaraka,pamoja na kuwafikisha mahakamani maofisa waandamizi wa Idara ya kilimo wilayani humo kwa tuhuma hizo.

No comments:

Post a Comment