Monday, August 13, 2012


                                                            CUF CHAMLIPUA DC GEITA
                                                            ADAIWA KUONGOZA KIBABE
                                                            AWATIMUA WANANCHI OFISINI KWAKE

                                                      Mkuu wa mkoa wa Geita Said Magalula
Na Daniel Limbe,Geita
CHAMA cha wananchi CUF wilayani geita mkoani hapa kimemshitaki mkuu wa wilaya hiyo Omary Manzie kwa mkuu wa mkoa wa huo Said Magalula kwa madai ya kutawala kibabe,kushindwa kutatua kero za wananchi na kuwabagua wananchi wake kwa itkadi za vyama vyao kinyume cha sheria.
 
Hatua hiyo imetokana na malalamiko mbalimbali ya wananchi ambayo yamekuwa yakiwasilishwa kwake kwa ajili ya kuyapatia ufumbuzi lakini baadhi yao huwatimua ofisini mwake kwa madai hana nafasi ya kusikiliza majungu.
 
Katibu wa Chama cha wananchi CUF wilayani geita Sevelin Malugu ameliambia NIPASHE kuwa Mkuu wa wilaya hiyo aliteuliwa na rais Jakaya Kikwete hivi karibuni kwaajili ya kuwatumika wananchi wa wilaya ya geita lakini hali hiyo imekuwa kinyume na matarajio ya wengi kwa kuwa amekuwa limbukeni wa madaraka,hali inayosababisha watu kuhoji sifa za kuteuliwa kwake.
 
“Mimi namuona DC wangu huyo ni limbukeni wa madaraka… kama nafasi aliyonayo anakuwa hivyo,je angepewa ukuu wa mkoa ingelikuwaje..ama angelikuwa kwenye cheo cha mheshimiwa Kikwete si angeliweza kutemea mate watu”alihoji Malugu.
 
Kutokana na hali hiyo Katibu huyo amemwandikia walaka wa maandishi mkuu wa mkoa huo (Magalula ) kuingilia kati mgogoro wa ardhi dhidi ya wananchi wa kijiji cha Nyantorontoro “A” na baadhi ya viongozi Idara ya madini wilayani humo ambao wanadaiwa kumilikisha ardhi ya wananchi kinyume cha sheria.
 
Katika taarifa ya Chama hicho mwekezaji aliyemilikishwa ardhi hiyo kinyume cha sheria ni Majaliwa Maziku, ambaye anadaiwa kufanya mazungumzo na viongozi wa idara hiyo kisha kumpatia eneo hilo licha ya wananchi wa maeneo hayo kudai hawajaripwa fidia ya ardhi yao .
 
Awali eneo hilo lilikuwa likimilikiwa na wananchi na baadaye mwaka 2004 ardhi hiyo ilichukuliwa na kampuni ya kichina ya  Sino Hidro Company Limited, iliyokuwa ikitengeneza barabara kwa kiwango cha lami kutoka wilayani Geita hadi Buzirayombo wilayani Chato kwa makubaliano ya kuitumia ardhi hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu ya mradi huo kisha ingelejea mikononi mwa wananchi hao.
 
Katika mradi huo wananchi hao walitakiwa kuhama maeneo hayo ili kuepuka kupata madhara yatokanayo na shughuli za ulipuaji baruti na vumbi kubwa linalotokana na usagaji wa kokoto kwenye “Crasher” ambapo wananchi hao walilipwa fedha kidogo kwa makubaliano ya miaka mitatu huku wengine wakikosa hata kiasi hicho cha fedha.
 
Hata hivyo baada ya mradi huo kuanza kutekelezwa baadhi ya wananchi walijitokeza na kupeleka malalamiko yao kwa mtendaji wa kjiji cha Nyankumbu kudai kulipwa fidia ya mazao na nyumba zao zilizoharibiwa baada ya milipuko iliyotokea septemba 8 mwaka 2006 kutokana na maeneo yao kutokuwa kwenye orodha ya watu waliolipwa awali.
 
Hatua hiyo ilipelekea mtendaji wa kijiji hicho kumwandikia barua mkuu wa wilaya hiyo Septemba 11 mwaka 2006 ikimuarifu Malalamiko ya kuharibiwa mazao kutokana na milipuko inayotokana na wachina wanaotengeneza barabara ya Geita hadi Buzirayombo,na baadaye Ofisi ya mkuu wa wilaya kuandika barua yenye Kumb. Namba.R. 40/1/VOL.V/147 ya novemba 8 mwaka 2006 kwenda kwa Meneja wa Tanroads Mkoa wa mwanza juu ya uwepo wa malalamiko hayo.
 
Aidha baada ya mradi huo kukamilika mwaka 2007 wananchi walilejea kwenye maeneo yao ya awali na kuendesha maisha yao ya kila siku lakini katika hali ya kushangaza hivi karibuni walipewa taarifa kupitia ofisi ya madini wilayani humo kuwa maeneo hayo yamemilikishwa kwa mwekezaji na kutakiwa kuondoka kwa kuwa tayari walishalipwa fidia ya ardhi zao na kampuni ya Kichina iliyokuwa ikitengeneza barabara.
 
Alipotakiwa kuzungumzia malalamiko hayo Ofisa madini wa kanda ya ziwa Juma Kharuna alikiri eneo hilo kugawiwa kwa mwekezaji na kudai kuwa taratibu zote za kisheria zimezingatiwa kwa kuwa eneo hilo lilikaa wazi kwa muda mrefu mpaka hapo alipojitokeza mwekezaji huyo.
 
Kadhalika Kharuna alimtaka mwandishi wa habari hizi kufanya mawasiliano na Mtendaji wa kata ya Kalangalala Hamad Juma ili kuzungumzia suala hilo kwa kina kutokana na kuufahamu vizuri mgogoro huo wa wananchi dhidi ya serikali.
 
Hata hivyo baada ya mwandishi wa habari hizi kumtafuta kwa njia ya simu mtendaji huyo alikanusha kuwa taarifa sahihi na badala yake kumuomba mwandishi wa habari kumtafuta mkuu wa wilaya kwa kuwa mgogoro huo ulishafika ofisini kwake.

 

No comments:

Post a Comment