Saturday, October 27, 2012

                           WALIMU SENGEREMA WATWANGANA MAKONDE OFISINI.

Na Daniel Limbe,Sengerema
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida,walimu wawili wa shule ya msingi Igaka wilayani Sengerema mkoani mwanza wametwangana makonde ndani ya ofisi ya shule baada ya kurushiana maneno makali kutokana na mwalimu mkuu msaidizi kumtuhumu mwenzake kwa uwajibikaji mbovu.

Akizungumza na NIPASHE mwalimu mkuu wa shule hiyo Boniphace Shilunga amesema tukio hilo limetokea juzi oktoba 19 mwaka huu majira ya saa 8 mchana baada ya mwalimu Lazimani Manyabele kusukumiana makonde na mwalimu mkuu msaidizi Edson Kagusa.

Hatua hiyo ilitokana na majibizano ya maneno kati ya walimu hao wawili baada ya mwalimu mkuu msaidizi kumtuhumu mwenzake kuwa ni amekuwa akivunja sheria za kwa makusudi kutokana na kuchelewa kufika shuleni na kushindwa kuhudhuria kwenye vipindi kama alivyopangiwa.

Amesema baada ya kurushiana maneno ndani ya ofisi hiyo mwalimu Manyabele alinyanyuka mahari alipokuwa ameketi na kumkwida mwalimu mwenzake baada ya kumwita kuwa msaliti hatua iliyosababisha kumrushia konde lililopelekea majibizano ya ngumi hizo kabla ya walimu wengine kuingilia na kuwaachanisha.

Amedai kuwa mbali na sheria za nchi zinazowataka watumishi kuwahi kazini na kutimiza wajibu wao,shule hiyo tayari ilikuwa imejiwekea utaratibu wa walimu wote kufika shuleni kabla ya saa 2 asubuhi sanjari na kuhudhuria kwenye vipindi vyote vya masomo ikilinganishwa na ilivyokuwa awali ambapo walikuwa wakifika shuleni saa 4 asubuhi na kuondoka pasipo utaratibu unaotakiwa.

Mratibu elimu kata ya Buzilasoga Robert Cheyo amekiri kuwepo kwa tukio hilo na kudai kuwa tayari amekwisha andaa taarifa ya maandishi kwenda kwa ofisa elimu wa wilaya hiyo ili hatua za kinidhamu zichukuliwe dhidi ya walimu hao kwa madai kupigana maeneo ya shule ni kuidhalilisha shule na taaluma ya ualimu.
Amesema kamwe serikali haiwezi kulifumbia macho suala hilo kwa kuwa ni utovu wa nidhamu kazini na uzalilishaji wa taaluma ya ualimu kwa kuwa wao wanatakiwa kuwa kioo kwa jamii wanayoiongoza.

Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya sengerema Juma Mwanjombe aliupoulizwa na mwandishi wa habari hizi kuhusiana na tukio hilo alidai kuwa tayari ofisi yake imekwisha pokea taarifa ya sakata hilo huku akiahidi kuwachukulia hatua kali za kisheria walimu hao ili iwe fundisho kwa wengine wenye nia ya kama hiyo.

Mwanjombe alifafanua kuwa walimu hao wamevunja sheria namba 56 ya mwaka 2003 ambayo inawataka walimu kuwa na mahusiano bora kazini na kwamba inabainisha wazi kuwa atakaye vunja sheria hiyo adhabu yake ni kupewa onyo kali,kutelemshwa daraja la kazi,au kufukuzwa kazi.

Aidha ametoa wito kwa walimu wote wilayani humo kutii sheria na kuheshimiana kwa kuwa ndiyo silaha ya mahusiano kazini na kwamba serikali haitamwonea aibu mwalimu yoyote atakaye endelea kuvunja sheria zilizowekwa kwa mujibu wa Katiba.

No comments:

Post a Comment