Saturday, October 27, 2012

    DIWANI WA NGEREJA AGEUKA OMBAOMBA,APORWA GEST NGUO,SIMU NA FEDHA

Na Daniel Limbe,Sengerema
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida diwani wa kata ya Kasenyi wilayani sengerema mkoani mwanza Sindano Sanyiwa amegeuka omba omba baada ya watu wanaosadikiwa vibaka kumpora nguo,simu ya mkononi na fedha zote alizokuwa nazo.
Sakata hilo limemkumba jana majira ya saa 8 usiku akiwa amelala kwenye chumba namba 105 kwenye nyumba ya kulala wageni ya Nyakaduha Motel iliyopo nje kidogo ya mji wa sengerema wakati akihudhulia vikao vya baraza lahalmashauri hiyo.
Hatua ya diwani huyo kugeuka ombaomba imekuja baada ya mwenyekiti wa halmashauri hiyo Methew Lubongeja kumpa nafasi ya kuuliza swali kwenye kikao cha baraza la madiwani,ambapo diwani huyo kabla ya kuuliza swali aliomba kulijulisha baraza hilo kuwa ameibiwa nguo zake,simu ya mkononi na fedha zilizokuwa kwenye mfuko wa suluali yake.
Kutokana na hali hiyo aliwaomba madiwani wenzake kufanya harambee ili kumsaidia kupata kiasi cha fedha zitakazomwezesha kuendelea kumudu gharama za maisha wakati akiendelea na vikao vya baraza hilo hatua iliyopelekea madiwani hao kubwaga vicheko vingi kabla ya mwenyekiti wao kuwatuliza.
“Mheshimiwa mwenyekiti kwanza kabisa napenda kulijulisha baraza lako tukufu kuwa usiku wa kuamkia leo nikiwa nimelala kwenye chumba changu kuna watu wanaohisiwa kuwa ni vibaka walikata nyavu za dirisha la chumba hicho kisha kuniibia nguo zangu,simu ya mkononi na pesa taslimu nilizokuwa nazo,hivyo ninaomba madiwani wenzangu mnichangie changie kiasi chochote ili nami niendelee kushiriki na ninyi kwenye vikao vyetu”alisema Diwani huyo.
Hata hivyo mwenyekiti wa baraza hilo alifanikiwa kutuliza vicheko vilivyoambatana na makofi ndani ya ukumbi huo na kuwataka madiwani kumpa pole mwenzao kwa tukio hilo kwa kuwa linaweza kumtokea mtu yeyote pasipo kujali ni kiongozi.
Baada ya hatua hiyo diwani huyo aliendeliendelea na swali lake la msingi juu ya ujenzi wa barabara ya Kafundile kwenda kasenyi Rugongo yenye urefu wa kilomita 17 na daraja la Shitwego linaloungaisha vijiji vya Kasenyi na Rugongo ambalo limekatika na kuwafanya wakulima wa maeneo hayo kushindwa kusafirisha mazao yao kwenda kwenye soko kuu la mjini sengerema.
Vilevile alidai kuwa kutokana na hali hiyo baadhi ya wakulima,mama wajawazito na wazee wamekuwa wakilazimika kutembea umbali mrefu kwaajili ya kufika kwenye soko kuu,hospitali ya wilaya na huduma zingine mhimu za kibinadamu zinazopatikana mjini sengerema.
Alidai kuwa licha ya barabara na daraja hilo kutangazwa na halmashauri hiyo kwaajili ya kumpata mkandarasi hakuna hatua zozote zilizoonekana kuchukuliwa ili kunusuru maisha ya wananchi wa kata ya Kasenyi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakilalamikia hali hiyo.
Kufuatia madai ya diwani huyo kuporwa mali zake NIPASHE limelazimika kufika kwenye Motel hiyo ili kupata ufafanuzi wa tukio hilo ambapo mbali na kukiri kuwepo kwa tukio hilo Meneja wa Motel hiyo Tindos Pangani amesema hatua hiyo imetokana na uzembe wa diwani huyo kwa kile alichodai alifungua dirisha na kuliacha wazi wakati akitaka kulala usiku.
“Tukio hilo lipo limetokea majira ya saa 8 usiku,lakini ninachoweza kusema ni kuwa diwani mwenyewe ndiye mzembe kwa maana wakati amelala alifungua dirisha na kuliacha wazi baadaya kuona kuna joto kali ndani huku akiwa kafungulia feni, hali iliyosababisha vibaka kupata njia rahisi ya kujipatia fedha”alisema Pangani.
Pangani amesema tukio hilo limetokea kwa mara ya pili tangu kufunguliwa kwa Motel hiyo takribani miaka 3 iliyopita na kwamba mazungumzo ya upotevu huo dhidi ya mteja wao yamefanyika na kupata suruhu.

No comments:

Post a Comment